Vidokezo vya Jinsi ya Kutunza Pesa

Tafsiri:
en_US

Watu wengi barani Afrika wanatatizika kifedha kutokana na hali ngumu ya kiuchumi. Licha ya kuwepo na ongezeko la mshahara, ni asilimia ndogo tu ya watu wanaoweza kukimu gharama za dharura za kama shilingi elfu 50. Sababu kuu ya shida kama hii ni watu wengi kushindwa kuimudu bajeti vizuri. Katika makala haya, tutaangalia vidokezo bora vya bajeti unayopaswa kutumia leo ili kuzuia kuwa katika hali hii tata ya kifedha.

Kidokezo cha Bajeti #1: Tayarisheni Bajeti Pamoja

Ikiwa mpo kwenye ndoa, tunapendekeza mtayarishe bajeti pamoja. Hii ina maana kuwa, kila mwezi mnapaswa kuwa na mkutano wa familia ambapo mnajadili bajeti ya mwezi uliopita, na kisha kuandaa bajeti ya mwezi unaofuata. Lengo la kuwa na vikao hivi vya pamoja ni kuhakikisha kwamba mtakuwa katika nafasi nzuri ya kukagua jinsi mwezi uliotangulia ulivyoenda na jinsi mnaweza kurekebisha bajeti ya mwezi mpya. Ikiwa haujaoa, tunapendekeza upate mtu mwingine ambaye pia hajaoa au kuolewa ili awe kama mshirika wako wa uwajibikaji.

Kidokezo cha Bajeti #2: Bajeti ya Msingi wa Sufuri (Zero-Based Budgeting)

Hii ni mbinu ya bajeti ambayo hutumiwa kawaida na kampuni lakini bado inaweza kutumika katika mazingira ya familia. Katika zero based budgeting, unaanza bajeti yako kutoka mwanzo kwa msingi wa sufuri. Lengo la kutumia njia hii ni kuhakikisha kuwa unashughulikia gharama zote katika familia yako kadiri mwezi unavyoanza. Kumbuka kujumuisha vitu kama akiba na gharama nyinginezo (miscellaneous) katika bajeti yako. Kama familia, unapaswa kuunda bajeti yako kila wakati kwa njia ambayo unaweza kuhifadhi pesa kila mwezi. Hazihitaji kuwa nyingi. Gharama nyinginezo zinapaswa kuwepo ili zikidhi mahitaji ambayo yanaibuka, kwa vile huenda hayakujumuishwa kwenye bajeti.

Kidokezo cha Bajeti #3: Anza na Mambo Muhimu Kwanza

Vitu katika bajeti ya familia yako vinapaswa kuorodheshwa kulingana na umuhimu wavyo. Kama familia, kuna mambo ambayo haiwezekani kuishi bila. Baadhi ya vitu hivi vya kimsingi ni kama kodi ya nyumba, chakula, mavazi na mafuta ya gari. Kuna mambo mengine ambayo unaweza kuishi bila kugharamikia kama vile televisheni za kulipiwa, intaneti, mavazi mapya (hauhitaji kununua nguo kila mwezi) na kutoa kwa uhisani (charity). Kwa kuiwekea kipaumbele bajeti yako, itakusaidia kujua wapi kupunguza gaharama na wapi kuongeza matumizi.

Kidokezo cha Bajeti #4: Jiepushe na Kadi Yako ya Mkopo (Credit Card) ya Benki

Credit card zimeharibu familia nyingi. Kadi hizi hutumia pesa ambazo sio zako bali unazokopeshwa. Usijenge tabia ya kutumia kadi hizi. Hii ni kwa sababu ya kuwa na tabia ya kununua vitu ambavyo huvihitaji, haswa wakati unapitiza kiwango cha bajeti yako. Hali hii huishia kuzifanya familia kujiingiza katika madeni yanayoweza kuepukika. Kwa hivyo, njia nzuri ya kuzuia kuchukua deni kubwa la kadi ya mkopo ni kutozitumia.

Kidokezo cha Bajeti #5: Kuwa na Mkutano wa Katikati ya Mwezi

Kampuni zina mikutano kadhaa kila mwezi, ambapo hukutana ili kupanga mikakati na kutathmini maendeleo ya mipango yao. Kama familia ni muhimu kuwa na mikutano hii ili kuwawezesha kufuatilia maendeleo ya bajeti na kufanya mabadiliko yanayofaa. Kwa hivyo, tunapendekeza muwe na mkutano wa katikati ya mwezi ambapo utakagua maendeleo hadi sasa. Huu unapaswa kuwa mkutano mfupi ambapo unaona ikiwa unafuata bajeti na kisha kufanya mabadiliko husika.

Kidokezo cha Bajeti #6: Yafuatilie Matumizi Yako

Hapo zamani, tungependekeza kwamba utumie wino na karatasi kufuatilia matumizi ya bajeti yako. Licha ya kuwa unaweza kufanya hivyo bado, tunapendekeza utumie zana nyinginezo za mtandaoni ambazo zinafuatilia matumizi yako. Programu hizi zitakupa taarifa wakati unazidi bajeti yako na pia kukuambia ni wapi unaenda kombo. Ukiwa na programu hizi, utakuwa na wakati rahisi wa kufuatilia matumizi yako ya kihistoria (ya awali). Baadhi ya programu bora unazoweza kutumia ni pamoja na Mipango Finance.

Kidokezo cha Bajeti #7: Fanya Matumizi Yawe Chini ya Bajeti

Bajeti ni zana tu ambayo hutoa msingi wa kile unachokusudia kutumia. Kila inapowezekana unapaswa kujaribu kila wakati kuweka akiba kutokana na bajeti yako. Kwa mfano, ikiwa umepanga kutumia shilingi elfu 10 kwa mafuta ya usafiri kila mwezi na uishie kutumia elfu 8, hili linapaswa kuwa jambo la kukufurahisha mno.

Muhtasari

Kuwa na bajeti au kutoifuata ni makosa mawili makuu ambayo watu wengi hufanya. Utafiti wa hivi karibuni uligundua kuwa 1 kati ya watu 3 hawatayarishi bajeti. Ikiwa wewe ni mmoja wao, unapaswa kuanza kuunda bajeti leo. Kwa kufanya hivi itakusaidia kufanya maamuzi mazuri ya kifedha.